Ijumaa , 30th Aug , 2019

Mkuu wa Mkoa Mbeya, Albert Chalamila, amesema wananchi ambao walishambulia msafara wa Mkuu wa Wilaya ya Kyela Claudi Kitta, wamechagua kuuawa, kwa kile alichokieleza wao walionesha nia ya kumuua Mkuu huyo wa Wilaya.

RC Chalamila ametoa kauli hiyo kata ya Ghana, jijini Mbeya ikiwa siku chache baada ya Msafara wa Mkuu wa Wilaya ya Kyela kushambuliwa na wananchi wa Kijiji cha Mpunguti.

RC Chalamila amesema kuwa "kwa sababu walirusha mawe na walichagua kumuua Mkuu wa Wilaya (Kyela) na Kamati ya Ulinzi na Usalama, hawa wamechagua kuuawa wao, na hili nalisema sio kinyume cha haki za binadamu haki za binadamu walipaswa kuwa nayo wao".

"Nawaambieni ukweli hapa bado sijafungua kikosi kingine, tunasubiri watu waaanze tena ili tupige king'ora cha mwisho." amesema Chalamila.

Mapema jana Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoani Mbeya Jeromi Ngowi, alisema jeshi hilo linaendelea na uchunguzi ili kuweza kuwabaini wale wote  waliohusika na kuvamia msafara wa Mkuu wa wilaya ya Kyela Claudi Kitta,  katika Kijiji cha Mpunguti wilayani humo.