Jumatano , 13th Jul , 2022

Waziri wa Maliasili Balozi Dkt.Pindi Chana, amewaagiza viongozi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro na TANAPA kuimarisha vikosi vya ujenzi ili vifanye ukarabati wa mara kwa mara wa miundombinu ya barabara na kushughulikia kwa haraka changamoto za kuharibika kwa miundombinu.

Katikati ni waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Dkt. Pindi Chana

Balozi Dkt. Pindi Chana ametoa agizo hilo wilayani Karatu mkoani Arusha, wakati wa ufunguzi wa barabara ya Seneto Crater katika hifadhi ya Ngorongoro akieeleza kuwa ukarabati wa barabara hiyo ni muhimu na utawafanya watalii wanaotembelea hifadhi hiyo wafurahie vivutio vya utalii katika msimu huu wa wageni wengi.

"Natambua ongezeko la wageni limeleta somo kubwa la mahitaji ya maboresho ya miundombinu ya barabara hasa barabara ya kutoka geti la Loduare hadi Golini, tunashukuru kwa kupata Fedha za Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano Dhidi ya UVIKO - 19  ambazo baadhi ya fedha hizo zilielekezwa kwenye matengenezo ya barabara hii ambayo tayari yamekamilika," amesema Balozi Dkt.Chana.

Licha ya kuipongeza Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) kwa kazi nzuri iliyofanyika ambayo italeta tija katika kupunguza gharama na kuongeza mvuto katika eneo hilo ameitaka  ieendelee kuzifanyia maboresho barabara nyingine ndani ya hifadhi hiyo.