Jumapili , 2nd Mei , 2021

Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeteketeza nyavu haramu zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 70 katika eneo la Migori, halmashauri ya wilaya ya Iringa kama sehemu ya mkakati kabambe wa kukabiliana na changamoto za uvuvi haramu katika bwawa la Mtera.

Nyavu haramu zilizoteketezwa

Akizungumza baada ya kuhitimisha zoezi la siku 10 la kusaka watu wanaofanya uvuvi haramu, kiongozi wa zoezi hilo Godbless Msuya, amesema katika zoezi hilo wamebaini idadi kubwa ya wavuvi wameanza kuhama katika eneo hilo kutokana na kupungua kwa samaki katika bwawa la Mtera tatizo ambalo limekuwa likichagizwa na uvuvi usiozingatia taratibu za uvuvi endelevu na salama.

Kwa upande wake Katibu Tawala wa wilaya ya Iringa Estomin Kyando, aliyezungumza kwa niaba ya mkuu wa wilaya ya Iringa ametoa rai kwa wananchi katika maeneo hayo kuendelea kutoa ushirikiano kwa mamlaka husika ili kumaliza changamoto ya matumizi yaa dhana haramu za uvuvi.