Jumamosi , 19th Jul , 2014

Serikali kupitia idara ya  uvuvi mkoani  mara  imeendesha  oparesheni  kali  na kufanikiwa kukamata  zana haramu  ambazo zilikuwa zikitumika  kuvulia  samaki  katika  ziwa  Victoria

Sehemu ya nyavu haramu zikiteketezwa kwa moto

Serikali kupitia idara ya  uvuvi mkoani  mara  imeendesha  oparesheni  kali  na kufanikiwa kukamata  zana haramu  ambazo zilikuwa zikitumika  kuvulia  samaki  katika  ziwa  Victoria  zenye  thamani  ya  zaidi  ya  milioni Tisini  kisha  kuziteketeza  kwa  moto.
 
Akizungumza  wakati  wa  kuteketeza  zana  hizo  haramu  za  uvuvi  katika  zoezi  ambalo limefanyika  nje kidogo  ya  mji  wa  musoma, kaimu afisa  mfawidhi  doria  na udhibiti  wa  uvuvi kanda ya mara  Bw Alli Mzee Said, amesema jumla  ya zana haramu  11,397  zimekamatwa  katika opareshini  hiyo.
 
Amesema  katika  oparesheni hiyo ambayo imedumu kwa siku 21  na kuhusisha wilaya za Rorya, Butiama na Bunda, jumla ya  makokoro  ya  dagaa  na  samaki  aina  ya  sangara 155 na kamba zake za kuvulia kokoro mita 39,205 zimekamatwa  pamoja  na  nyavu 11,242 ambazo  haziruhusiwi  kisheria kuvulia   samaki pia zimekamatwa. 
 
Kwa upande wake kaimu mkuu wa wilaya ya musoma Bw John Henjewele, akizungumza baada ya kuwasha moto kwa ajili ya kuteketeza zana hizo haramu, amesema serikali haina nia ya kuwafilisi wavuvi na wafanyabiashara wa nyavu, bali wanapaswa kuzingatia sheria na kwamba  zoezi hilo linakuwa endelevu katika kupambana na uvuvi haramu katika ziwa Victoria.

Nao baadhi ya  wakazi  wa  mkoa  wa  mara Bw  David Katikiro na Bw Emmanuel Bwimbo, pamoja na kuipongeza serikali  kwa jinsi inavyopambana  na uvuvi haramu  katika  ziwa  Victoria, lakini pia  wamesema  kuna  haja kwa serikali  kuchukua hatua  ya  kudhibiti uingizaji  wa  zana  hizo  kutoka nje  ya  nchi, hatua ambayo  wamesema  itasaidia kupambana na  uvuvi huo  haramu