Jumatatu , 1st Apr , 2024

Mwili wa mtu mmoja ambaye haujafahamika jina umeokotwa akiwa amepoteza maisha pembeni mwa barabara inayoelekea Dodoma kutoka Kiteto eneo la Kijiji cha Partimbo.

Mwili wa mtu ambaye hajafahamika kwa haraka ukiwa pembezoni mwa barabara

Mwenyekiti wa Kijiji cha Partimbo Kimirey Masiaya amethibitisha kifo hicho akisema hakuna mtu aliyetambua mwili huo na kwa sasa umehifadhiwa chumba cha kuhifadhi maiti Hospitali ya wilaya ya Kiteto.

EATV imezungumza na baadhi ya mashuhuda ambapo mmoja wa shuhuda aliyeshuhudia mwili huo amesema majira ya asubuhi wakati wanapita na mifugo kwenda kunywesha maji walimuona yule bwana yuko pale na haikuwa rahisi kumsogelea hivyo walimwangalia na wakapita kwa mbali.

"Tulijaribu kumwita hakuitika tukiwa na mifugo tukawaacha watu hapo wakapiga simu Polisi wakati tunarudi na mifugo tukakuta Askari Polisi tukawapa ushirikiano lakini ni mtu ambaye hatumjui" amesema Baraka sisime   

"Niliambiwa mtumishi kuna mtu kalala barabarani njoo ikabidi niende tukamwona mtu amejikunja amelala nilipomwangalia nikaona ni mtu amefariki nikawaambiwa watu watoe taarifa kituo cha polisi wakaja kushuhudia lakini hatujajua sababu ya mtu yule kufa" amesema Hezeroni Kirura Mchungaji wa Kanisa

"Mimi nilikuwa napita tu hapa wakati natoka nyumbani huko juu wakati naenda kijiweni kufika hapa nikaona watu wamejaa kuangalia nikaona Polisi walikuwepo wakasema kuna mtu amefariki"Joseph  yohana Mwananchi Partimbo