Alhamisi , 10th Jul , 2014

Jeshi la Polisi Mkoani Dodoma linamshikilia mwalimu wa shule ya sekondari ya Hombolo, Justus Jackson mwenye umri wa miaka 28, kwa tuhuma ya kumuua mwalimu mwenzie kwa kukataa kulipa shilingi elfu moja ya bili ya umeme aliyotakiwa kuchangia marehemu.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma David Misime.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Dodoma, David Misime amemtaja mwalimu aliyeuwawa kuwa ni Fredy Ndahani (29) mwalimu wa shule ya Hombolo.

Misime amesema walimu hao wote wawili wanalikuwa wakiishi katika nyumba moja na walikuwa wakichangia bili ya umeme katika nyumba hiyo.

Amesema katika mabishano walimu hao waliingia katika ugomvi na hivyo Fredy alisukumwa katika ukuta na kupoteza maisha papo hapo.

Kwa mujibu wa kamanda Misime, mtuhumiwa huyo ameshakamatwa na anatarajiwa kufikishwa mahakamani mara baada ya kukamilika kwa upelelezi.

Wakati huo huo, majeruhi sita kati ya nane wa asili ya Kiasia, waliojeruhiwa vibaya sehemu za miguuni, baada ya kurushiwa bomu la kurusha na mkono usiku wa Julai 8 mwaka huu, wakiwa kwenye mgahawa wa Vama Traditional, uliopo eneo la uzunguni, wameruhusiwa.

Akizungumza kwa njia ya simu, mkurugenzi wa tiba na Kaimu Mganga Mkuu wa hospitali ya Seliani, Dk, Paul Kisanga, amesema majeruhi waliopo wodini hadi sasa ni wawili tu ambao ni Deepak Gupta, aliyekatwa mguu wa kushoto na Prateek Javey.

Amewataja majeruhi walioruhusiwa ni Vinod Suresh, Ritwik Khandehral, Raj Rajin, Manci Gupta, Manisha Gupta na Mahish Gupta.