Jumanne , 29th Jun , 2021

Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa amezindua rasmi mpango  wa tatu wa maendeleo ya taifa wa miaka mitano huku akiwahidi watanzania kuwa mambo yote yaliyoahidiwa katika kampeni za mwaka 2020 yatatekelezwa na mpango huo.

Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa

Mhe. Majaliwa amezindua mpango huo leo Juni 29, 2021, jijini Dodoma akimuwakilisha Makamu wa Rais wa Tanzania Dkt. Philip Mpango nakueleza kuwa fedha zitapopatikana na malengo ya mpango huo  yatafikiwa kwa asilimia mia na zaidi.

“Nataka niwaahidi watanzania kwamba mambo yote tuliyowaahidi katika kampeni 2020 yanaendelea kutelekelezwa kupitia mpango huu na utekelezaji wa mpango wa tatu unatarajia kugharimu jumla ya shilingi trillion 114.8 “ amesema Waziri Majaliwa.

Aidha, akielezea safari  yake ya maendeleo Mhe. Majaliwa amemshukuru Rais Mstaafu wa awamu ya nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania DKt. Jakaya Mrisho Kikwete kwa kumuanzishia safari yake ya kisiasa.

“Nitumie nafasi hii kumshukuru Mhe. Jakaya Kikwete ndiye aliyenianzishia kufanya kazi utumishi ndani ya serikali, alinitoa darasani nakunipa ukuu wa wilaya kwa mara ya kwanza 2005, na nilipohudumu nikajikimbiza kwenda jimboni na kuwa mbunge, akaniteua kuwa Naibu Waziri wa Elimu nafasi niliyodumu kwa miaka 5, uwepo wangu hapa jukwaani na uwepo wake chini kwangu  lazima niringie kwani ana mchango mkubwa katika maendeleo yangu,” amesema Waziri Mkuu.

Hata hivyo katika kuhakikisha mpango huu unatelekezwa Waziri Mkuu ameziagiza taasisi za umma, idara zinazojitegemea, na wadau wote wa maendeleo kuhakikisha ofisi zao zote zina mpango huu ili kuwezesha utekelezaji kwa pamoja na viwango.