Jumatatu , 9th Feb , 2015

Madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Njombe wamemuagiza mkurugenzi kusimamia kikamilifu idara ya elimu wilayani humo kufuatia kushuka kwa ufaulu wa wanafunzi wa shule za misingi mwaka jana.

Mkuu wa Mkoa wa Njombe Dkt. Rehema Nchimbi

Wakizungumza kwenye kikao cha baraza madiwani hao wamesema ufaulu umeshuka kwa kiasi kikubwa kutokana na afisa elimu msingi na mkurugenzi kushindwa kuwasimamia waratibu elimu na walimu kwa kuwa walimu hao hawakai kwenye vituo vyao vya kazi wakijishughuluisha na kilimo pamoja na kupanda miti ya mbao.

Pia katika kikao hicho kumeibuka malalamiko kwa mkurugenzi kuwa ameshindwa kusimamia utoro wanafunzi ambapo zaidi ya wanafunzi mia moja katika shule ya msingi lole kata ya ikuna wametoroka shuleni na kusababisha migongano baina uongozi wa kata na shule hiyo

Akijibu tuhuma kwa niaba ya mkurugenzi afisa elimu msingi wilaya ya Njombe Hamisi Milowe pamoja na kukiri kuwa ufaulu umeshuka amebainisha changamoto zinazo pelekea ufaulu kushuka kuwa ni upungufu mkubwa wa walimu pamoja na utoro uliokithiri kwa wanafunzi.

Awali akifungua kikao hicho mwenyekiti wa halmashauri hiyo Valency Kabelege amesema kuwa idadi kubwa ya wanafunzi waliofaulu kujiunga kidato cha kwanza mwaka 2015 hawajawasili mashuleni na kuwataka wazazi na walezi pamoja na viongozi kusimamia.