Jumapili , 18th Aug , 2024

Mbunge wa jimbo la Simanjiro Christopher Ole Sendeka, ameiomba kampuni iliyopo kijiji cha Kandaskira ambayo inaendeleza ujenzi wa kiwanda cha kuchakata madini ya kinywe wilayani humo kutoa kipaumbele cha ajira kwa wanajamii wanaozunguka kiwanda hicho na pia ili wanufaike na CSR.

Mbunge wa jimbo la Simanjiro Christopher Ole Sendeka

Kauli hiyo ameitoa wakati ambapo Waziri wa Madini Anthony Mavunde alipofika kiwandani hapo kwa ajili ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa kiwanda cha kuchakata madini hayo cha Permanent Minerals Ltd na kusema Tanzania kwa sasa ni ya tatu katika uzalishaji wa madini ya kinywe katika bara la Afrika, ikitanguliwa na Madagascar na Msumbiji.

"Tunaamini kwamba leseni 10 zote za kati na kubwa za uchimbaji madini kinywe zikianza kufanya kazi nchi yetu itakuwa miongoni mwa nchi vinara wa uzalishaji madini kinywe Afrika," amesema Waziri

Kwa upande wake mmoja wa wamiliki wa kiwanda hicho God Mwanga, amesema kiwanda kikikamilika kitakuwa na uwezo wa kuchakata tani 108,000 kwa mwaka na kitatoa ajira 300 za moja kwa moja huku Halmashauri ya Simanjiro ikitegemewa kuongeza mapato kupitia uwekezaji huo.