Ijumaa , 16th Mei , 2014

Mbio za mwenge wa uhuru nchini zimekuwa na manufaa mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuhamasisha mapambano dhidi ya ugonjwa wa malaria nchini

Kiongozi wa mbio za mwenge Racheal kassanda akikabidhi mwenge kwa makamu wa Rais Dkt Bilal wakati wa uzinduzi wa mbio hizo mwezi April mwaka huu mjini Bukoba

Kiongozi wa mbio za Mwenge wa uhuru mwaka huu Rachel  Stephen Kassanda amewataka watanzania kuongeza vita dhidi ya ugonjwa wa Malaria kutokana na ugonjwa huo kuongoza kwa kusababisha vifo vya wananchi hasa watoto walio chini ya umri wa miaka mitano.
  
Kassanda ametoa wito huo kwa nyakati tofauti wakati akizundua miradi mbalimbali ya maendeleo wakati wa mbio za Mwenge wa uhuru katika manispaa ya Kigoma Ujiji, ambapo amesema kila mwananchi ana wajibu wa kuhakikisha anapambana na ugonjwa huo,

Kasanda pia amewataka watendaji wa serikali kuhakikisha wananchi wana elimishwa na kupatiwa matibabu stahiki.
 
Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Kigoma Ramadhan Maneno amesema ujenzi  wa ofisi za kata katika manispaa hiyo zilizozinduliwa na kiongozi wa mbio za Mwenge zitaongeza ufanisi katika kazi.

Nao baadhi ya vijana waliohudhuria sherehe hizo wameitaka serikali kuongeza mapambano dhidi ya rushwa na utawala bora pamoja na mikopo kwa vijana.