Alhamisi , 23rd Oct , 2014

Serikali mkoani kigoma imeyafunga machimbo madogomadogo ya dhahabu katika kata ya Nyamtukuza wilaya ya Kakonko mkoani Kigoma, kutokana na kudaiwa kuwa chanzo cha mauaji yaliyotokea mwishoni mwa wiki

Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Luten Kanal Mstaafu Issa Machibya

Serikali mkoani kigoma imeyafunga machimbo madogomadogo ya dhahabu katika kata ya Nyamtukuza wilaya ya Kakonko mkoani Kigoma, kutokana na kudaiwa kuwa chanzo cha mauaji ya watu watatu yaliyotokea mwishoni mwa wiki kufuatia ugomvi wa kugombea ardhi katika kijiji cha Minyinya.
 
Akihutubia wananchi katika kijiji cha Minyinya, Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Luten Kanal Mstaafu Issa Machibya amesema, uchunguzi wa awali umeonesha kuwa chanzo cha mapigano kati ya wakulima na wafugaji ni machimbo ya dhahabu  ya Kanyomvi, Nyamwilonge na Lutela yaliyopo katika kata hiyo ambayo yaliwavutia watanzania kutoka mikoa ya Shinyanga na Geita kuhamia katika kijiji hicho kwa lengo la kuchimba dhahabu na baadae wakaleta mifugo na kuanza kulima katika mashamba ambayo yanadaiwa kuwa ni wananchi wa kijiji hicho, na kwamba serikali imelazimika kuyafunga ili kuepusha maafa zaidi.
 
Kwa upande wao, wananchi wa kijiji cha minyinya kata ya nyamtukuza, wamesema kwa muda mrefu wamekuwa wakipata mateso kutoka kwa jamii ya wafugaji inayoishi katika maeneo wanayolimia kutokana na wao kuyatumia mashamba yao kinyume cha utaratibu, hali ambayo imesababisha mapigano na watu kuyakimbia maeneo yao , ambapo wameiomba serikali kuwaondoa.
 
Mapigano kati ya wakulima na wafugaji yalitokea katika kijiji cha minyinya mwishoni mwa wiki na kusababisha watu watatu kuuawa na kuchomwa moto.