Ijumaa , 13th Mei , 2022

Serikali imesema itaendelea kuongeza jitihada katika mapambano dhidi ya vitendo vya ukatili kwa wanawake na watoto kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo pamoja na wizara husika ili kuhakikisha makundi hayo yanakuwa salama.

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, Dkt. John Jingu akiwa na Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Dkt. Zainab Chaula

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Dkt. John Jingu, wakati akiongoza kikao cha kamati elekezi ya Mpango kazi wa Taifa wa kutokomeza ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto (MTAKUWWA) kilichofanyika Jijini Dodoma na kuhudhuriwa na Makatibu Wakuu, wawakilishi kutoka Wizara mbalimbali na wadau wa maendeleo nchini.

Katibu Mkuu huyo alisema ipo haja ya kuongeza nguvu katika mapambano hayo kila mdau kwa nafasi yake ili kuongeza jitihada za utekelezaji wa mpango huo kutokana na kuongezeka kwa vitendo na matukio ya ukatili katika maeneo mbalimbali.

"Inabidi tuongeze nguvu yaani serikali, Wizara za kisekta , Idara,Taasisi, Asasi za kiraia,wadau  na vyombo vya ulinzi katika mapambano haya wote kwa nafasi zetu ili kuongeza kazi ya utekelezaji wa mpango huu na kufikia hilo lazima tuwe na rasilimali kulinda na kutetea makundi ambayo yamekuwa yakiathirika kutokana na vitendo hivyo,” amesema Dkt. Jingu.

Pia ameongeza kwamba kwa mujibu wa muongozo wa maandalizi ya mpango na bajeti ya serikali kwa mwaka wa fedha 2022/2023 unaelekeza kutengwa kwa fedha kwa ajili ya kutekeleza afua za MTAKUWWA huku akiziomba taasisi na wadau kuona namna ya kuongeza rasilimali kufikia malengo ya serikali ya kukomesha vitendo vya ukatili.