Ijumaa , 16th Feb , 2018

Kamanda wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Jeshi la Polisi (SACP), Lazaro Mambosasa amewatadhahalisha watu kujiepusha na vitendo vya kihalifu ili waweze kuruhusu uchaguzi wa marudio ufanyike kwa amani na utulivu.

Kamanda Mambosasa ametoa wito huo leo (Ijumaa) wakati alipokuwa anazungumza na waandishi wa habari Kinondoni Jijini Dar es Salaam na kusema Jeshi la Polisi wamepata taarifa za kiuchunguzi kuwa kuna kundi la watu wachache kutoka katika chama kimoja cha siasa ambao wamepanga kufanya vurugu kwenye uchaguzi unaotarajiwa kufanyika kesho (Jumamosi) katika Jimbo la Kinondoni.

"Jeshi la Polisi limejipanga vizuri, uchaguzi uliopita 2015, tulikuwa na majimbo kadhaa ndani ya Dar es Salaam lakini kwa huu wa marudio tuna jimbo moja tu hili la Kinondoni na kwa sababu hiyo ni seme kwamba Jeshi la Polisi tumejipanga imara na kuhakikisha hakuna mtu atakayeruhusiwa kuingia na kufanya vurugu kwenye uchaguzi", amesema  Kamanda Mambosasa 

Pamoja na hayo, Kamanda Mambosasa ameendelea kwa kusema "nimeambiwa kwamba kuna mabaunsa lakini sijawahi kupata baunsa anayeweza kupambana na serikali halafu akabaki na ubansa wake. Namuonea huruma huyo baunsa aliyejiandaa kupambana na dola, niwashauri tu kuwa mtu haishi kwa kifua kikubwa bali anaishi kwa kutii sheria. Yeyote atakae fanya vinginevyo ajue hatobaki salama".

Kwa upande mwingine, Kamanda Mambosasa amesema ni vyema kwa mtu yeyote ambae ameshawishiwa kufanya vurugu katika zoezi la kupiga kura ni bora akijitoa mwenyewe kuliko kuingia katika matatizo kwa sababu hakuna atakayeachwa akafanya fujo kisha akaendelea kupiga hatua mbele.