Ijumaa , 6th Sep , 2024

Watu wasiojulikana wanadaiwa kuwalawiti na kuwachoma na kitu kinachodhaniwa kina ncha kali mama na mtoto wake katika mtaa wa Muungano Kata ya Mkonze Jijini Dodoma.

Mama na mtoto

Wakizungumza na vyombo vya habari eneo la tukio mashuhuda ambao ni majirani wa eneo hilo wamesema mama huyo anakadiriwa kuwa na umri wa miaka 33 na mtoto wake anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 11 wamekutwa wamefariki wakiwa na majeraha baadhi ya maeneo ya miili yao ndani ya nyumba waliyokua wanaishi eneo la Mkonze Jijini Dodoma.

Mama huyo anayejulikana kwa jina la Mwavita  Mwakibasi na Binti yake Salma Silvesta inadaiwa wamefanyiwa ukatili huo usiku wa kuamkia leo Alhamisi tarehe 06.09.2024.

Mtoto mkubwa wa Marehemu jina limehifadhiwa kwa uchungu mkubwa amesema  aliamshwa na mdogo wake na kumwambia mama yao anavuja damu hali iliyomsukuma kupiga simu kwa bibi yake ili waweze kupata msaada wa haraka huku dada wa marehemu akisema alipata taarifa ya tukio hilo kupitia simu ya mama yao aliyepo Jijini Mbeya.

Mwenyekiti wa mtaa huo amekemea matendo hayo ya kikatili yanayoendelea katika mtaa wa Mkonze na kuliomba Jeshi la Polisi kuweka kituo ambacho kitasaidia kutoa huduma za kiuaalama kwa haraka zaidi kwani eneo hilo kwa sasa linakua kwa kasi.

Lazaro Mbishe Kaimu Kitengo cha Mawasiliano Hospitali ya Mkoa wa Dodoma amethibitisha kupokea mwili mmoja wa mwanamke na mtoto 1 ambaye alikua mahututi ambaye alifariki wakati akipatiwa matibabu.