Jumanne , 16th Jul , 2024

WATU wawili wamefariki dunia papo hapo na mwingine kulazwa Hosptali,kufuatia magari ya kubeba mizigo aina ya HOWO waliokuwa wakisafiria kutoka na kwenda Mikoa ya kusini na Kaskazini kugongana uso kwa uso kwa uzembe unaodaiwa kufanywa na mmoja wa madereva hao.

Kwa mujibu wa taarifa ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Lindi ACP John Imori ajali hiyo imetokea eneo la Kijiji cha Mkwaya,barabara kuu Lindi Mtwara Julai 14 mwaka huu saa 8:50 mchana.

Amewataja madereva waliofariki Daudi Augustino Mdota (44) wa Kampuni ya Saruji ya Dangote Mkoa wa Mtwara na Jafari Abdull Omari (39) wa Kampuni ya Speciallzed Haulers Ltd,inayobeba makaa ya mawe.

Imori amesema Saidi Mussa (22) ni abairia aliyekuwa anasafiri na Gari la Speciallzed Haulers Ltd amelazwa Hosptali ya Sokoine mjini Lindi akiwa hoi taabani kutokana na malori hayo kuungua kasha kuteketea kabisa na moto.

Amesema Daudi Augustino Mdota alikuwa anaendesha Lori lenye Namba za usajili T 234 DZT kutoka Dar es salaam kwenda Mtwara na Jafari A,Omari akiendesha Lori namba T 132 DUJ mali ya kampuni ya Specialallzers Ltd kutoka Mtwara kwenda Jijini Dar es salaam.

Imori ametaja chanzo cha ajali ni uzembe uliofanywa na dereva wa kampuni Dangote kutoka upande wa kushoto kwenda kulia na kukutana na Lori la kampuni ya Speciallers Ltd uso kwa uso na kulipuka moto.

"Baada ya haya magari kugongana uso kwa uso yamewaka moto na kuteketea yote mawili papo hapo"Alieleza Kamanda Imori.

Kamanda huyo wa Polisi Mkoani Lindi amewataka madereva kuwa makini wanakuwa wanaendesha vyombo vya moto ili kuepusha ajali kwa wananchi wengine,wakiwemo wanaotembea kwa miguu.

Mganga mfawidhi Hosptali ya Sokoine Dr Alexandaer Makalla amekili kumpokea abiria huyo akiendelea na matibabu na kueleza bado hali yake sio mzuri sana kutokana na majeraha ya moto aliyoyapata.

Mmoja wa abiria aliyekuwa anasafiri na Lori la Dangote kutoka Mnazi mmoja Lindi kwenda Mtwara ambaye hakupenda jina lake litajwe kwenye vyombo vya Habari (Issa Juma) anamshukuru mungu baada ya kushushwa njiani na dereva wa Lori hilo baada ya kumueleza angesimama kumuangalia mwendesha Pikipiki aliyekuwa amemsukumu na kuanguka.

"Nikiwa mnazi mmoja nilipanda Gari la Dangote kwenda Mtwara, tulipofika kijiji cha Mkwaya,dereva akamsukuma mwendesha pikipiki na kuanguka chini bila kusimama,nilipomshauri asimame ili akamuangalie akaamua kunishusha"Alisema Abiria huyo.

Abiria huyo akasema baada ya Lori hilo kutembea umbali mfupi akagongana na Lori la kubeba makaa yam awe na kulipuka moto na kuteketea yote mawili.