Ijumaa , 30th Aug , 2024

Israel imekubali kusitisha mapigano kwa siku tatu mfululizo ili kuruhusu kusambazwa kwa misaada ya kibinadamu huko Gaza.

Shirika la Afya Duniani (WHO) limesema Israel imekubali mfululizo wa kusitishwa kwa mapigano ili kusambaza misaada ya kibinadamu huko Gaza ili kuruhusu chanjo ya watoto dhidi ya polio, 

Kampeni hiyo italenga kutoa chanjo kwa watoto 640,000 katika ukanda wa Gaza na itaanza siku ya Jumapili, afisa mwandamizi wa WHO Rik Peeperkorn amesema.

Itatolewa katika hatua tatu tofauti, katika sehemu za kati, kusini na kaskazini mwa ukanda. Katika kila hatua, mapigano yatasitishwa kwa siku tatu mfululizo kati ya saa 06:00 na 15:00 kwa saa za huko.

Makubaliano hayo yanakuja siku chache baada ya maafisa wa Umoja wa Mataifa kusema mtoto wa miezi 10 amepooza kwa sehemu baada ya kuambukizwa ugonjwa wa kwanza wa polio katika ukanda wa Gaza kwa miaka 25.

Karibu dozi milioni 1.26 za chanjo ya polio ya mdomo aina ya 2 (nOPV2) tayari ziko Gaza, na dozi 400,000 za ziada zinatarajiwa kuwasili hivi karibuni.