Alhamisi , 1st Aug , 2024

Naibu Waziri Mkuu Tanzania Dotto Biteko amewataka wachama wa Chama cha wanasheria wa Tanganyika TLS kuhakikisha kuwa wanachagua viongozi bora wenye uwezo wa kushauri na kukosoa huku wakiweka mbele taaluma zao za sheria

Biteko ameyasema hayo leo wakati akifungua mkutano mkuu wa TLs ulioenda sambamba na maadhimisho ya miaka 70 tangu kuanzishwa kwake

"TLS mnalo jukumu kama chama kuchagua viongozi watakaoendeleza mshikamano wa chama chenu, watakaokuwa na kiu ya kuishauri na wakati mwingine kuikosoa serikali, jambo ambalo mmekuwa mkilifanya, naamini mtakuwa na viongozi ambao watakuwa na matamko ya kitaaluma, nitoe wito kwa chama kuendelea kuwa na msisitizo wa kukaa kwenye taaluma yenu kama wanasheria"  - Dotto Biteko, Naibu Waziri Mkuu wa Tanzania 

Aidha amesema kuwa serikali itaendelea kushirikiana bega kwa bega na chama hicho katika masuala mbalimbali ya kisheria nchini 

"Leo tunaadhimisha miaka 70 ya kuanzishwa kwa TLS, hili sio suala dogo ni jambo kubwa la kupongezwa, zipo taasisi nyingi zilizoanzishwa baada ya kuanzishwa kwake zilikufa nyingine mwaka mmoja, miwili na nyingine kumi lakini TLS imeendelea kuwepo kwa miaka 70"

"Serikali imekubaliana na nyinyi na Rais amekuwa mfano mzuri wa kuwapa kila aina ya nyenzo  mnayohitaji, mmeomba ardhi amewapatieni, Dodoma mmepata, Arusha mmepata, mnatamani kufanya mambo makubwa, Rais amenituma niwajulishe kuwa kila jambo mnalokusudia kulifanya yupo pamoja na nyinyi"