Jumatano , 6th Dec , 2017

Mwenyekiti wa CHADEMA Wilaya ya Kinondoni, Waziri Muhunzi amesema hawana hofu juu ya aliyekuwa Mbunge wa jimbo hilo Maulid Mtulia (CUF) kuhamia CCM kwani wako imara na wanasubiri taratibu za kutangazwa siku ya uchaguzi ili waweze kutetea kiti hicho.

Kauli hiyo imetolewa leo Jumatano na alipokuwa akituma salamu kwa wananchi wa jimbo la  kuwataka kuwa wavumilivu baada ya aliyekuwa Mbunge wa jimbo hilo Maulid Mtulia kujiuzulu uongozi mwishoni mwa wiki iliyopita.

"Wananchi wa Jimbo la Kinondoni wako salama kwani Mtulia hakuondoka na wanachama hivyo tuko vizuri na hatujasambaratika kama ilivyodaiwa hapo awali. Ikitokea wanachama wanaandamana na wao kurudi CCM basi tutajua tatiazo liko wapi. Hapa tulipo tunasubiri tu Tume ya Uchaguzi itangaze ni lini uchaguzi ili tuingie kazini," amesema Muhunzi.

Ameongeza "Lazima tulitetee jimbo hili na uzuri aliyekuwa Kampeni Meneja wa Mtulia 2015 ni mimi hapa na sijahama kwa hiyo lazima tuhakikishe jimbo linabaki kwenye mikono ya upinzani. Mbunge wa jimbo hili bado ataendelea kutoka UKAWA licha ya usaliti aliyoufanya Mtulia ili hali CHADEMA ilipigania kila hatua kuhakikisha amepata nafasi hiyo katika uchaguzi wa 2015.

"CCM hawako salama wasifikiri kumchukua Mtulia wamemaliza Wilaya ya Kinondoni, wanachama wapo na wataendelea kuwepo ndani ya CHADEMA," amesema.