Jumanne , 20th Jan , 2015

Chama cha Mapinduzi CCM,kimesema hakitasita kuwachukulia hatua kali za kimaadili wanachama na viongozi wa chama hicho ambao wameendelea na kampeni za kuwania nafasi za juu za chama hicho ikiwemo ile ya urasi kabla ya wakati.

Katibu wa Itikadi Uenezi wa CCM Nape Nnauye

Pia chama hicho kimewatahadharisha juu ya usambazaji wa taarifa zisizosahihi kwa hofu ya kuchukuliwa hatua na kuwataka kujidhibiti na kudhibiti wapambe wao.

Akiongea na vyombo ya habari mjini zanzibar, katibu wa itikadi uenezi wa chama hicho Nape Nnauye amesema kuwa chama hakitasita kuchukua hatua kali kwa wanachama na viongozi ambao wameendelea kukaidi agizo la kamati kuu la kuwataka kutojihusha na kampeni kabla ya wakati.

Aidha Nape amesema kuwa chama kimewataka wanachama na viongozi hao, kuwadhibiti wapambe wao ambao wamekuwa wakitoa taarifa potofu pindi vikao vya kamati kuu inapoketi na kusema kuwa chama hicho kina kazi nyingi za kufanya si kujadili wagombea pekee.

Kuhusu kamati ya maadili iliyoketi tarehe Januari 19, 2015 Nape amesema kuwa mambo yote yaliyojadiliwa katika kamati hiyo yatawasilishwa kwenye kamati kuu kwa kujadiliwa na ndipo yatatolewa kwa wananchi na kuwataka wagombea kutokuwa na hofu kama wanahisi wako sahihi kimaadili.