Alhamisi , 16th Oct , 2014

Kamati kuu na Halmashauri Kuu ya chama cha Mapinduzi {NEC} zimekutana mjini Dodoma ambapo pamoja na mambo mengine vikao hivyo vimejadili mchakato wa Bunge la Katiba.

Kamati kuu na Halmashauri Kuu ya chama cha Mapinduzi {NEC} zimekutana mjini Dodoma ambapo pamoja na mambo mengine vikao hivyo vimejadili mchakato wa Bunge la Katiba na kubainisha maafakiano ya upatikanaji wa katiba mpya kati ya Rais Jakaya Kikwete na vyama vya siasa vinavyounda kituo cha Demokrasia Tanzania {TCD} hayazuii chama hicho kuendelea na mchakato wa katiba.

Vikao hivyo vikuu vya CCM mbali na kujadili mchakato wa Bunge Maalum la Katiba pia vimezungumzia mustakabali wa chama hicho katika chaguzi zijazo za serikali za mitaa na uchaguzi mkuu huku katibu wa itikadi na uenezi wa chama hicho Nape Nnauye akisema wataendelea kujadili katiba kwani ajenda za TCD sio ajenda za CCM kwa kuwa vikao vyake vinajitegemea na viko huru.

Akizungumzia msimamo wa chama hicho kuhusu kura za maoni ya wananchi Nape amesema CCM itaendelea kuheshimu sheria ya mabadiliko ya katiba ya mwaka 2012 sura ya 83 inayoelekeza kura za maoni zipigwe ndani ya siku 84 baada ya bunge maalum kuvunjwa lakini pia akisisitiza sheria hiyo inaweza kufanyiwa mabadiliko na Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.