Alhamisi , 8th Apr , 2021

Baba mzazi wa kijana Kusekwa George mkazi wa mtaa wa Ihushi kata ya Kishiri, Nyamagana Mwanza, amekataa kuhudhuria msiba na shughuli ya kuaga mwili wa mwanaye huyo mwenye miaka 17.

Jeneza lenye mwili wa kijana Kusekwa George

Mzee George amekataa akishinikiza mwili wa kijana huyo anayedaiwa kuuawa kwa kupigwa na Mwenyekiti wa mtaa pamoja na Sungusungu, upelekwe kwa Mwenyekiti kisha amrejeshe mwanaye akiwa hai.

Kwa upande wa wakazi wa mtaa wa Ihushi kata ya kishiri wilayani Nyamagana mkoani Mwanza wamesema hawatauzika mwili wa kijana Kusekwa George.

Wakazi wa mtaa wa Ihushi wakiwa msibani

Wananchi wamedai kuwa kijana huyo aliuawa kwa kupigwa na marungu, fimbo pamoja na mkanda wa mashine na mwenyekiti wa mtaa akishirikiana na Sungusungu.

Wananchi hao leo Aprili 8, 2021, wameupeleka mwili wa kijana Kusekwa nyumbani  kwa Mwenyekiti huyo ili amrudishie uhai wake.