Jumatano , 13th Apr , 2016

Mtu mmoja wa Kata ya Majengo katika manispaa ya Moshi, Mkoani Kilimanjaro, Edward Hussein, amefariki dunia baada ya kusombwa na maji katika eneo la Njoro kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro Wilbroad Mutafungwa

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Wilbroad Mutafungwa, amesema tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia jana ambapo bado haijafahamika mtu huyo alikua anaelekea maeneo gani.

Amesema mtu huyo ambaye anakadiriwa kuwa na umri wa kati ya miaka 35 hadi 40 mkazi wa Majengo ambaye mwili wake umehifadhiwa katika hospitali ya Mawenzi alikutwa kwenye korongo lenye maji akiwa ameshafariki dunia.

Nao baadhi ya wakazi wa Moshi wameiomba serikali ya mkoa kurekebisha miundombinu ya barabara ikiwemo kuzibua mitaro yote iliyoziba ili kupunguza maafa yasiendelee kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha.