Jumanne , 1st Dec , 2015

Jeshi la Polisi nchini linawashikilia maafisa 12 wa Mamlaka ya Mapato (TRA) kwa tuhuma za utoroshwaji wa makontena 349 bandarini kufuatia uchunguzi uliofanywa na wataalam waliobobea katika uchunguzi wa makosa ya uhalifu wa kifedha wa jeshi hilo.

Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, CP Diwani Athumani

Akiongea na vyombo vya habari Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, CP Diwani Athumani. amewataja baadhi ya maafisa wa TRA wanaoshikiliwa kuwa ni pamoja na Tiagi Masamaki ambaye ni Kamishna wa Idara ya Forodha na Ushuru, Habibu Mponezia Meneja Kitengo cha Ushuru, Eliachi Mrema Msimamizi Mkuu Kitengo cha Forodha, Haroun Mpande Kitengo Mawasiliano (ICT) na Hamis Omary Mchambuzi Mwandamizi wa Masuala ya Biashara TRA.

CP Athumani amesema kuwa watuhumiwa wengine majina yao hayajatolewa kwa sasa kutokana na sababu za upelelezi, na kusema kuwa jeshi la polisi linatarajia kukamilisha uchunguzi wao mapema iwezekanavyo na kuwafikisha mahakamani mara moja watumishi hao wa TRA.

Aidha DCI, Athumani ametoa wito kwa wale wote waliohusika na ubadhrifu wa fedha za Umma kujisalimsha wenyewe kwa jeshi la polisi kwa kuwa msako unaofanywa kwa vyovyote vile watabainika.