Jumatatu , 2nd Sep , 2024

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Mohamed Mchengerwa amewaagiza Wakala wa Mabasi yaendayo haraka(DART), kutoa nafasi kwa wawekezaji nchini kwa ajili ya kuweka Mabasi ili kupunguza kero ya usafiri kwa jiji la Dar es Salaam, ifikapo Disemba 2024.

Mohamed Omary Mchengerwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, akizindua mfumo mpya wa ukataji tiketi

Waziri Mchengerwa ameyasema hayo wakati anazindua mfumo wa kukusanyia nauli wa kisasa leo kwenye kituo cha mwendokasi Kimara mwisho jijini Dar es Salaam.
"Washirikisheni wazabuni wa kitanzania wapo wengi wana uwezo wa kuleta mabasi ambayo yanaweza kupunguza changamoto mfano Mabasi ya kwenda Morogoro sasa  hivi mengi hayana abiria wamiliki wanaweza kupewa tenda ya kubeba abiria wa mwendokasi, sio lazima wawe abiria wa nje ya nchi",  Mohamed Mchengrwa.

Mwenyekiti wa Bodi ya DART anaelezea namna mfumo huo utakavyorahisisha huduma kwa wananchi.
"Mfumo huu utaondoa usumbufu wa chenji kwa abiria , lakini pia utapunguza foleni ya watu kukaa muda mrefu kwenye madirisha lakini pia tunaendelea kuboresha mifumo ili kurahisisha huduma kwa wananchi", alisema Dkt.Florence Tuluka.

Baadhi ya watumiaji wa usafiri wa mabasi hayo wanasema ilikuwa inawalazimu kuacha chenji inapotokea wana haraka.
"Kwanza tutaondokana na kuacha hela zetu maana umeenda sehemu nauli 750 unafika dirishani wanasema hawana hamsini ukipiga mahesabu ni hela nyingi kwahiyo tukikata kwa mfumo hela zetu zitaokoka", alisema  Godfrey Majani, Abiria wa mwendokasi.

"Kuna siku nilisubiri chenji mpaka gari likaniacha kwa sababu hawakuwa na chenji sasa hii imekuwa kama tabia na hatujui kama kweli hawana chenji au walikuwa wanatufanyia kusudi",alisema  Fatma Makwawa, Abiria wa mwendokasi.