Wednesday , 23rd Oct , 2024

Wawekezaji kutoka mataiafa mbalimbali wamekaribishwa nchini Tanzania kwa ajili ya kuwekeza kwenye sekta ya Nishati jadidifu ya Joto Ardhi ili kuongeza vyanzo Vya uzalishaji wa Umeme nchini.

Wito huo umetolewa na Makamu wa Rais wa Tanzania Dokta Philip Isdor Mpango, kwenye ufunguzi wa kongamano la 10 la nishati jadidifu ya Joto Ardhi kwa nchi za Afrika uliofanyika leo jijini Dar es Salaam.

"Tanzania ipo tayari kwaajili ya uwekezaji katika sekta ya jotoardhi kutokana na kuwa na amani na utulivu, mazingira mazuri ya kuvutia, utulivu wa kisiasa pamoja na sera imara chini ya marekebisho ya kimuundo kupitia falsafa ya R nne za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ambazo ni mageuzi, kujenga upya, maridhiano na ustahimilivu, baadhi ya maeneo muhimu ambayo yatazalisha nishati ya jotoardhi ni pamoja na Ngozi (Megawati 60), Kyejo – Mbaka (Megawati 60), Songwe (Megawati 5-35), Natron (Megawati 60) na Luhoi (Megawati 5)"DKT.PHILIP MPANGO-Makamu wa Rais Tanzania.

Nao mawaziri kutoka Tanzania bara na Visiwani Zanzibar wanaelezea umuhimu wa kuongeza vyanzo Vya uzalishaji nishati kwa Taifa.

“Tunalo deni kufikia Disemba kila kijiji kiwe na umeme nchini kwahiyo kuongezeka kwa vyanzo Vya nishati ni muhimu sana kwa ajili ya Taifa letu na mataifa mengine”, KAPTENI GEORGE MKUCHIKA-Waziri wa Ofisi ya Rais

“Zanzibar tunategemea umeme kutoka Tanzania bara tunatumia megawat 150 lakini mahitaji yetu kwa sasa ni makubwa kwahiyo ni muhimu nchi ya Tanzania kuwa na vyanzo vingi vya uzalishaji nishati ya Umeme", SHAIB  KADUARA -Waziri wa Maji, Nishati na Madini Zanzibar.

Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Daniel Chongolo anasema Songwe wana eneo la kuzalisha Umeme huo kwa megawatt 4, huku Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila akielezea namna alivyokomesha wizi wa mafuta ya Transfoma.

"Sisi Songwe tuna eneo la maji moto ambalo mradi ukianza tutazalisha megawatt 4, na sisi tupo tayari kupokea mradi huu a tumeshafanyiwa utafiti na mradi huu utasaidia kulinda misitu n utasaidia kupata nishati kwa gharama nafuu", DANIEL CHONGOLO- Mkuu wa Mkoa wa Songwe

"Hali ya kukatika kwa umeme katika moa wa Dar es Salaam ilikuwa inasababishwa pia na baadhi ya watu kuiba transfoma za umeme na kuchukua mauta yaliyomo ndani ya transfoma, lakini baadhi ya wezi waliokamatwa walilazimishwa kunywa mafuta hayo", ALBERT CHALAMILA-Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam.