Monday , 7th Oct , 2024

Vyombo vya Dola mkoa wa Dar es Salaam, vimetakiwa kuhakikisha vinadumisha amani hasa kuelekea katika Uchaguzi wa Serikali za Mtaa ili uchaguzi uweze kuwa huru na haki.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila wakati anakabidhi Pikipiki 30 kwa Jeshi la Polisi kwa ajili ya kuongeza ufanisi wa kazi yao.

“Novemba 27, 2024 hapa hatuaombi vyombo vya dola kubadilisha matokeo hapana bali tunaviomba vikajiimarishe ili watakaoshindwa kukubaliana na matokeo washughulikiwe, tunawaomba sana
tunapoelekea uchaguzi wa Serikali za
mtaa shughuli zetu ziendelee kama
kawaida, Tumesikia kuna watu huwa wanaleta watu mkoa wa Dar es Salaam kwa ajili ya kutisha watu, halafu baadae kuonekane uchaguzi umevurugika na haukua wa haki, ili uchaguzi uwe na kiashiria cha demokrasia lazima uwe huru na wa haki, vyombo vya dola vitusaidie mazingira ya uhuru na haki kuelekea uchaguzi, ili wachache wenye nia mbaya wakisema uchaguzi haukua huru na haki isionekane Rais amesababisha, kuna umuhimu wa kuhakiksha mambo yanakuwa sawa”, alisema Albert Chalamila, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam.

Kwa upande wake Kamanda wa Jeshi la Polisi kanda maalum ya Dar es Salaam, SACP Jumanne Muliro, anasema watahakikisha wanaimarisha ulinzi kupitia vifaa walivyopatiwa.
“Tutatumia Pikipiki hizi katika Shughuli za kisiasa na kiraia ziweze kufanyika sawasawa Kumekuwa na maboresho makubwa sana katika kuzuia vitendo vya kihalifu kwahiyo tuna ahidi hilo”, alisema Sacp Jumanne Muliro, Kamanda Kanda Maalum ya Dar es Salaam.

Nae Mkuu wa wilaya pamoja na Meya wa Kinondoni wameliomba Jeshi hilo kushiriki katika kikamilifu katika uchaguzi huo.
“Makamnda wote uchaguzi wa Serikali za mtaa ni uchaguzi muhimu sana, niombe tujitokeze kwa wingi kwanza kujiandikisha ili muweze kupiga kura lakini pia mjitokeze kutusaidia kwenye uchaguzi kuhakikisha usalama unakuwepo kwenye maeneo yetu”, alisema  Saad Mtambule, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni.

“Sote tunatambua amani ya Dar ikivurugika inaweza kuambukiza mikoa mingine ndio maana wanasiasa wanajaribu kutumia mkoa huu kuharibu amani, matarajio yetu Pikipiki hizi zitazidisha amani na umoja kwenye jamii yetu”, alisema Songoro Mnyonge, Meya Manispaa ya Kinondoni.