Wednesday , 28th Aug , 2024

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Daniel Sillo ameipongeza Tasnia ya Uokaji Tanzania kwa kuwezesha Watanzania kupata chakula bora na salama kwa afya zao, kutokana na bidhaa za uokaji kuwa sehemu ya maisha yao hasa zikiwa bora na salama. 

Sillo ameyasema hayo leo Agosti 27, 2024 katika hafla iliyolenga kuwatambua watu  wanaofanya biashara ya Uokaji Tanzania ikiwa ni kwa mara ya kwanza kufanyika nchini sambamba na kugawa tuzo kwa wafanyabiashara wa Uokoaji, iliyoandaliwa na Umoja wa waokaji Tanzania (TBA) ambapo amesema kuwa Tasnia ya uokaji ni muhimu nchini hasa ikizingatia ubora na usalama wa chakula nchini, Pia bidhaa hizo hutumiwa na wananchi wa hali zote

“Hongereni kwa kutoa elimu kwa Waokaji ambao licha ya kutoa bidhaa za chakula pia watachangia  kukuza uchumi na pato la nchi kupitia biashara hio". Alitoa wito kushirikiana na TBA kuboresha Mazingira rafiki ya biashara na uwekezaji nchini 

Naye Mwenyekiti wa Umoja wa Waokaji Tanzania TBA, Francisca Lyimo ameeleza mafanikio waliyoyapata kutokana na umoja huo ulioanzishwa Mei 21, 2021 ukiwa na  lengo la kutetea watumiaji wa bidhaa za uokaji Tanzania. Miongoni mwa mafanikio ni kutoa elimu kwa watu 1500 ambao mpaka sasa wanajishughulisha na biashara hiyo.

Pia ameiomba Serikali kuangalia VAT iliyopo katika bidhaa za uokaji kama mkate iondolewe ili bidhaa hio ipatikane kwa urahisi na kutaja Vikwazo wanavyo kutana navyo ni kodi na tozo nyingi zinazowakwamisha wafanyabiashara wadogo hivyo biashara nyingi hukwama. 

Vilevile Mkurugenzi wa Biashara Azania Group of Companies, Joel Laiser ameeleza changamoto ambayo tasnia ya uokaji ilipitia kutokana na kupotea kwa dola nchini lakini kwa sasa hali imekuwa shwari, Pia  ametoa pongezi kwa Serikali ya awamu ya sita kwa kuboresha miundombinu ya barabara na upatikanaji umeme wa uhakika hivyo kuboresha shughuli za uokaji

"Kuna wakati sisi wafanyabiashara ya uokaji tulipitia changamoto zilizotokana na uhaba wa dola hadi kufanya bei ya ngano kuwa juu lakini kwa sasa hali ni nzuri, Pia tunaishukuru Serikali kwa kuboresha miundombinu ya barabara na umeme wa uhakika hivyo biashara ya uokaji imeimarika" Amesema Joel