Friday , 16th Aug , 2024

Wananchi kaya zaidi ya 200 wanaoishi mtaa wa Manzese Midizini, wameiomba Serikali kuwatatulia kero ya kukatika kwa maji zaidi ya mwaka mmoja hali inayopelekea kununua Maji kwenye madumu mbapo dumu moja wananunua shilingi 500 hadi 2000.

Wananchi wa Mtaa wa Midizini walia na kero ya Maji.

EATV ilifika mtaa huo na kushuhudia namna ambavyo wananchi wanapitia changamoto ya ukosefu wa Maji.
"Unakariia mwaka mmoja na nusu hatuna Maji, hivi kweli hii ni Manzese au tupo vijijini , mitaa mingine wana maji, sisi tumewakosea nini au sisi sio Watanzania maana zamani tulikuwa na maji ghafa yakakata mabomba yanatoa hewa, bili wanakuja kudai na maji hayatoki", alisema Iddy Dogoli, Mkazi wa Mtaa wa Manzese Midizini.

"Jifikirie tunanununa dumu moja shilingi 500 kuna kipindi tuna nunua mpaka 2500 kipindi ambacho kuna changamoto ya Maji jamani Dawasa wanatutesa sana na maji yenyewe tunayonunua robo tatu vumbi yani machafu mwisho wa siku tutauziwa maji ya chooni bila sisi kujua tunaom,ba Serikali itusaidie Maji ni Uhai", alisema  Felister Masamba, Mkazi wa Mtaa wa Manzese Midizini.

"Tunadamka alfajiri tunaacha wame zetu wamelala mwishowe tuachike maana hatukai na amani kila siku tunahangaika na kutafuta Maji, maumbile yetu wanawake yanahitaji maji sasa tutaishi mpaka lini maisha haya ya kukosa maji Serikali iko wapi?",  alisema Mariam Dismas, Mkazi wa Mtaa wa Manzese Midizini.

Mwenyekiti Mtaa wa Midizini ana lipi kuhusu changamoto hii?
"Ni kweli changamoto ipo na mimi kama mwenyekiti nimeshafanya jitihada mbalimbali kuhakikisha wananchi wanapata Maji lakini sikufanikiwa, ingawa DAWASA walinambia wana mradi ambao utatuletea kwenye mitaa ambayo tuna changamoto", alisema Abas Mrisho, M/Kiti Mtaa wa Manzese Midizini.

EATV Haikuishia hapo ikawatafuta DAWASA nao wamekiri kuwepo kwa changamoto kwenye baadhi ya mitaa ya Manzese pmoja na mabibo.
"Ni kweli kuna changamoto kwenye baadhi ya mitaa ya Manzese na mabibo lakini tupo kwenye mradi ambao upo zaidi ya asilimia 70 na tuna amini maeneo yote ambayo kwa sasa yanakutaa na changamoto hii inaenda kuisha kabla ya mwezi huu kwani tumeongeza mtandao kutoka Tanki letu la Kimara, kwahiyo niwaase wananchi wasiwe na wasiwasi muda si mrefu changamoto itaisha", alisema  Mhandisi Maria Samson, Mhandisi wa Maji mkoa wa kihuduma Magomeni.