Wednesday , 24th Jul , 2024

Katika mji wa Mtwara, ambao unajulikana kwa shughuli za uvuvi na rasilimali za gesi asilia, serikali imeamua kutoa mafunzo ya elimu ya fedha kwa wananchi, wajasiriamali, na watumishi wa serikali kwa lengo la kuwawezesha kujikomboa kiuchumi na kusimamia vyema rasilimali zao.

Wananchi

Mafunzo haya yalitolewa na Wizara ya Fedha kwa ushirikiano na taasisi za kifedha na wataalamu wa masuala ya fedha. Wananchi waliohudhuria mafunzo hayo walikuwa pamoja na wajasiriamali  wadogo wadogo, wafanyabiashara wadogo, na watumishi wa serikali waliotoka katika idara mbalimbali za mji.

Miongoni mwa washiriki alikuwa Bi. Mariam Kajewa mwanamke mjasiriamali anayejishughulisha na biashara ndogo ndogo. Kabla ya mafunzo, Mariam alikuwa na changamoto za kusimamia mapato yake na kudhibiti matumizi yasiyokuwa na tija. Baada ya kushiriki mafunzo, Mariam aliweza kujifunza mbinu za kuanzisha bajeti ya biashara yake, umuhimu wa kuweka akiba, na jinsi ya kutumia mikopo kwa njia yenye faida.

Kwa upande wa watumishi wa Serikali  Ofisa Mifugo, Michael Kigoso, mafunzo yatamsaidia kuboresha uwezo wake wa kusimamia mshahara wake kwa kuweka vipaumbele vya matumizi na kuchagua njia sahihi za kuweka akiba na kuwekeza.

Kwa pamoja, wananchi, wajasiriamali, na watumishi wa Serikali waliohudhuria mafunzo hayo watajikomboa kiuchumi kwa kuboresha usimamizi wao wa fedha. Walipata uelewa zaidi wa jinsi ya kutumia rasilimali zao vizuri, kuzuia madeni yasiyokuwa na tija, na kufanya maamuzi ya kifedha yanayowezesha maendeleo yao binafsi na ya jamii zao.

Kupitia elimu ya fedha, wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyamba mkoani  Mtwara walipata njia ya kuongeza mapato yao, kuweka akiba, na kushiriki kikamilifu katika uchumi wa mji wao. 

Serikali pia itanufaika kwa kuwa na watumishi walio na ujuzi wa kifedha ambao watakuwa na uwezo wa kusimamia rasilimali za umma kwa ufanisi zaidi.

Akizungumzia mafunzo hayo, Afisa Usimamizi wa Fedha  kutoka Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha - Wizara ya Fedha, Bi. Elizabeth Mnzava, alisema kuwa  mafunzo ya elimu ya fedha yaliyotolewa na Wizara ya Fedha yalikuwa ni muhimu sana katika kusaidia wananchi, wajasiriamali na watumishi wa Mtwara kujiinua kiuchumi na kufikia malengo yao ya kifedha.