Wednesday , 24th Jul , 2024

Sakata la utoro la kutokuonekana kambini kwa kiungo Mshambuliaji wa Simba SC Kibu Denis Prosper limezidi kuchukua sura mpya baada ya msimamizi wa mchezaji huyo Alpha Yazid kusema hajui alipo mchezaji huyo kwa sasa licha ya kupaswa kuwepo kambini mjini Ismailia nchini Misri.

Akizungumza kwenye mazungumzo maalum na EATV,Alpha Yazid amesema kama msimamizi wa mchezaji huyo hajui ni wapi alipo kwa sasa huku akiweka wazi adhabu zinazoweza kumpata pindi akishindwa kujiunga na kambi mpaka hivi sasa.

“hakuna namna yeyote ambayo Kibu anaweza kwenda kucheza klabu nyingine kama hajafanya mazungumzo na Simba , na hata kama anahitaji kuvunja mkataba anatakiwa kuanza kufanya mazungumzo na klabu yake ili wakubaliane kuvunja huo mkataba na alipe fedha ya kuvunja mkataba ambayo wamekubaliana wakati wakisaini mkataba mpya’’ Yazid Alpa Msimamizi wa Kibu Denis

Kwa upande mwingineYazid amemtaka mchezaji Kibu Dennis kuheshimu mkataba wake ndani ya Simba na kurejea mara moja ndani ya Simba huku kama kuna klabu inahitaji huduma yake inapaswa kuwasiliana na Simba SC ili kupata huduma ya mchezaji huyo

‘’kuna mfumo unaitwa FIFA Connect ili umsajili mchezaji unahitajika uombe ridhaa kwenye klabu aliyotoka ambayo haijaombwa na hakuna ofa yeyote ambayo imeletwa Simba, vinginevyo klabu ya Simba inaweza kuishitaki hiyo  klabu na itaomba fedha nyingi ambayo sidhani kwamba hiyo klabu kama itakuwa ipo tayari kuingia kwenye hasara ya  kulipa fedha nyingi kwaajili ya fidia” Yazid Alpha