Friday , 21st Jun , 2024

Ikiwa Tanga ndiyo kinara wa waraibu wa dawa za kulevya kwa hapa nchini serikali wilayani humo imesema ipo macho kuwachukulia hatua wale wote ambao wanajihusisha na uingizaji wa dawa za kulevya na kuiasa jamii kuendelea kutoa ushirikiano kwa vyombo vya ulinzi na usalama.

Dawa za kulevya

Katibu Tawala wa Wilaya ya Tanga Dalmia Mikaya amesema hayo wakati wa hotuba yake katika maadhimisho ya siku ya kupinga dawa za kulevya duniani yaliyofanyika kiwilaya kwenye kituo cha afya Mikanjuni.

Katibu Tawala huyo ameitaka jamii kuacha kutumia dawa za kulevya kwa rika zote kwani yanaleta athari na kupoteza nguvu kazi ya Taifa na kuwahamasisha wale waraibu waliofanikiwa kuacha matumizi ya dawa za kulevya, waanze kufanya shughuli za ujasiriamali kwa kuwa serikali imewatengenezea mazingira wezeshi. 

Mganga Mkuu wa Jiji la Tanga Dkt. Stephen Mwandambo amesema kuwa Jiji la Tanga linawapongeza wadau mbalimbali kwa kutoa elimu katika shule za msingi, sekondari na vyuo, taasisi za dini na kwenye makongamano ya kisiasa juu ya athari za dawa za kulevya kijamii, kiuchumi na kimazingira.