Thursday , 30th May , 2024

Watoa huduma za fedha mkoani Manyara wametakiwa kufuata sheria na taratibu za BoT ikiwemo kujisajili, kutoza viwango sahihi vya riba na kuwapa nakala za mikataba wakopaji baada ya wao kuelewa mkataba wa makubaliano ya kukopa na kusaini ili kuepuka adhabu mbalimbali zitakazotolewa kwa wanao

Agizo hilo limetolewa na Mkuu wa mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, ofisini kwake alipokutana na baadhi ya watumishi wa Wizara ya Fedha kabla hawajaingia kwenye kikao cha Baraza la Biashara lililofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara, kutoa elimu ya fedha kwa wajumbe wa kikao hicho.

Amesema kuwa serikali inaendelea kufanya uchunguzi kuwabaini wanaofanya biashara ya kutoa huduma za fedha bila leseni, ambapo baadhi yao wamekuwa wakikamatwa na kuadhibiwa huku akiwaonya wafanyabiashara wasiofuata kanuni, taratibu na sheria ya huduma za fedha kusajili biashara zao kupitia Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

"Wafanyabiashara wanaofanya biashara zao bila kujisajili, bila kufuata sheria, waache na Serikali ipo kazini tumekuwa tukiwakamata na tutaendelea kuwakamata na sheria itachukua mkondo wake," amesema RC Sendiga.

Aidha ameipongeza Wizara ya Fedha kwa kutoa elimu ya fedha katika mkoa wake kutokana na mkoa huo kuwa na uhitaji mkubwa wa elimu ya fedha, kwakuwa wananchi wengi wamekuwa wakijiingiza kwenye mikopo kwa wafanyabiashara wasio waaminifu na baadae kusababisha umasikini.