Tuesday , 7th May , 2024

Kocha mkuu wa Yanga SC Miguel Angel Gamondi amesema wamejipanga vizuri kuhakikisha wanapata alama tatu katika mchezo wa kesho jumatano ya Mei 07, 2024 katika uwanja wa Azam Complex Chamazi ili kuzidi kuweka matumaini makubwa ya kushinda taji la Ligi Kuu Tanzania Bara 2023-24.

Akizungumza na waandishi wa Habari,Kocha Gamondi amesema kuwa michezo yote ya mwisho wa msimu ndani ya ligi kuu inakuwa ni  michezo migumu lakini wataingia kucheza kama mchezo wao wa fainali ili kupata ushindi ili kulisogelea taji la ligi kuu Tanzania Bara msimu  2023-24.

"Tumejipanga vizuri kupata pointi tatu katika mchezo wetu kwani sisi kila mchezo kwetu ni fainali tunaomba mashabiki wetu waje kwa wingi uwanjani tunaahidi kupata pointi tatu, amesema  Gamondi.

Kwa upande mwingine, Kocha Msaidizi wa Kagera Sugar Marwa  Chamberi amesema wataingia kwa tahadhari kubwa kutokana na kuwa watakutana na timu yenye ubora wa hali ya juu msimu huu ndani ya Ligi Kuu Tanzania Bara.

Yanga SC ambao ni mabingwa watetezi wa ligi,wanashika nafasi ya kwanza wakiwa na alama za 65  huku imebakiza alama 8 kutangazwa kuwa mabingwa wapya wa ligi kuu Tanzania Bara 2023-24 huku wakiwa wamebakiza michezo 5 mpaka sasa.