Monday , 11th Apr , 2022

Uongozi wa Simba SC umethibitisha kuwa Kiungo Mshambuliaji kutoka nchini Ghana, Bernard Morrison hatokuwa sehemu ya msafara utakaokwenda Afrika Kusini baadae mwezi huu.

Simba SC itakwenda Afrika Kusini Juma lijalo kwa ajili ya mchezo wa mkondo wa pili Robo Fainali, Kombe la Shirikisho Barani Afrika dhidi ya Orlando Pirates.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Simba SC Barbara Gonzalez amesema: “Tuliwasiliana na watu wa Mamlaka za Uhamiaji Afrika Kusini kuomba kupata ruhusa ya kuingia na Morrison, walitueleza sheria zao mtu akivunja hawezi kupata tena nafasi ya kuingia,”

“Wametuambia kutokana na kosa lake mamlaka haipo tayari kumruhusu kutokana na sheria zilivyo, hivyo ni rasmi sasa Morrison hatakwenda Afrika Kusini.”

“Baada ya mechi dhidi ya Polisi Tanzania (iliyochezwa jana) tutamjulisha kocha ili afahamu hilo na kuona jinsi ya kujipanga kwa mechi wa ugenini bila ya Morrison.”

Simba SC itanzia nyumbani Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam Jumapili (April 17) kuikabili Pirates, kisha itakwenda Afrika Kusini kwa mchezo wa mkondo wa pili utakaopigwa Jumapili (April 24).