Friday , 25th Dec , 2015

Bei ya zao la korosho imeshuka kutoka sh. 2,700 kwa kilo moja mpaka kufikia sh. 2,450, hali ambayo imesababishwa na baadhi ya wanunuzi hapa nchini kukosa soko la zao hilo kimataifa.

kaimu meneja mkuu wa Chama Kikuu cha Ushirika cha Masasi-Mtwara na Nanyumbu (MAMCU), Kelvin Rajabu

Akizungumza na waandishi wa habari katika kikao cha kuelezea mchakato mzima wa biashara ya zao hilo unavyokwenda, kaimu meneja mkuu wa chama kikuu cha ushirika cha Masasi-Mtwara na Nanyumbu (MAMCU), Kelvin Rajabu, amesema korosho zinazokosa soko ni zile zinazopatikana kipindi hiki cha mwezi Desemba mpaka Januari.

Aidha, amesema sababu nyingine inayosababisha kuporomoka kwa bei katika kipindi hiki ni kutokana na kuanza kwa msimu wa korosho katika nchi nyingine za Afrika Magharibi ambazo ni mshindani wa kibiashara wa Tanzania.

Ameongeza kuwa wanunuzi wanaamua kwenda kununua huko kwa kuamini Tanzania msimu umekwisha wakati bado wakulima wanaendelea na kilimo cha zao hilo.