Friday , 7th Aug , 2015

Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) limesema serikali itaanza kuzalisha umeme wa gesi asilia inayotoka Madimba, mkoani Mtwara mpaka Kinyerezi, Dar es Salaam mwanzoni mwa mwezi Septemba mwaka huu.

Bomba ambalo litatumika kusafirisha Gesi kutoka Mtwara hadi Kinyerezi jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari jana baada ya kutembelea kiwanda hicho, Mkurugenzi wa TPDC, James Mataragio, amesema kabla ya kuisafirisha gesi hiyo kutakuwa na zoezi la majaribio kwa ajili ya kujiridhisha na ubora wa mitambo.

Mataragio amesema kuwa mchakato wa kuanza kuzalisha umeshakamilika baada ya siku mbili tatu wataanza majaribio ya kutiririsha gesi hiyo kabla ya kuanza uzalishaji kamili mwezi wa tisa.

Akizungumzia changamoto ya mmomonyoko wa udongo ambayo ilijitokeza Januari 13 mwaka huu katika eneo la mitambo ya kuzalisha umeme iliyopo Mnazibay, Mataragio amesema eneo hilo sasa liko salama na bado zoezi la kujaza mawe katika sehemu ambayo ilimomonyoka linaendelea.