Wednesday , 23rd Dec , 2015

Mabingwa watetezi wa ligi kuu ya soka Tanzania bara Young Africans wamesema mechi ya majaribio waliyocheza dhidi ya Friends Rangers ni sehemu ya kufanya marekebisho ya makosa yaliyojitokeza katika mchezo uliopita dhidi ya Stand United.

Kocha msaidizi wa Yanga Juma Mwambusi amesema pamoja na kushinda 4-0 dhidi ya Stand lakini kulikuwa na makosa yaliyojitokeza kwa wachezaji ambayo yalionekana na hata katika mchezo wa leo wa majaribio ambao Yanga waliweza kuibuka na ushindi wa bao 4-2 dhidi ya Friends pia wachezaji walikuwa wakifanya makosa katika mchezo huo.

Mwambusi amesema, sehemu ya ulinzi bado ni tatizo katika timu hiyo ambapo bado wanaendelea na mazoezi ili kuweza kufanya vizuri zaidi katika michezo mingine iliyombele yao.

Mwambusi amesema, pamoja na kurekebisha makosa lakini mchezo huo wa kirafiki pia umewasaidia kuweza kuangalia uwiano kati ya wachezaji wageni ambao wamesajiliwa katika klabu hiyo na wachezaji ambao wapo mda mrefu katika timu.

Kwa upande wa maandalizi ya muendelezo wa michuano ya ligi kuu ya soka Tanzania Bara ambapo Yanga watakutana na Mbeya City siku ya Jumamosi uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam, Mwambusi amesema wanajiandaa na timu zote 16 kuhakikisha wanapata point nyingi ili kuweza kutetea ubingwa walionao.

Mwambusi amesema, mpira hautabiriki na kikosi wanakiamini na wameamua kutengeneza kikosi kipana kutokana na mashindano mengi yaliyo mbele yao.