Thursday , 8th Jan , 2015

KLABU ya Yanga ya jijini Dar es salaam imetangaza rasmi kuachana na Mlinda Mlango Juma Kaseja, iliyemsajili kwa Sh. Milioni 40 Novemba 8 mwaka juzi.

Akithibitisha taarifa hizo, Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano, Jerry Muro amesema, hatua hiyo imefikiwa baada ya mchezaji huyo kuanza kujiengua katika timu.

Mwishoni mwa mwaka jana, Kaseja aliwasilisha barua kwa mwajiri wake, Yanga SC kutoa taarifa ya kuvunja mkataba wake uliokuwa umebakiza mwaka mmoja.

Katika Barua yake, Kaseja alisema sababu ya kuvunjwa mkataba huo ni kukiukwa kwa masharti yaliyokubaliwa wakati wa kusainiwa Novemba 8 mwaka jana.

Barua ya Kaseja iliyotumwa kupitia wakili wake, Mbamba & Co Advocates, Kaseja imesema wakati wa kusainiwa Mkataba huo ilikubaliwa malipo ya Sh. Milioni 40 yafanyike kwa awamu mbili.

Alisema awamu ya kwanza, alilipwa Sh. Milioni 20 baada ya kusaini Mkataba huo na ikakubaliwa fungu lililobakia alipwe Januari 15 mwaka jana na kwasababu malipo ya Fedha ndiyo msingi wa mkataba wenyewe, kushindwa kulipa Fedha hizo kunaondoa uhalali wake.

Baadaye Yanga ilikuja kusema imekwisha mlipa Fedha zake zote Kaseja na hana anachodai, ingawa Kipa huyo alifungua madai mapya, akidai anachukiwa na kocha wa Makipa, Juma Pondamali hivyo hana amani ya kufanya kazi.

Kaseja pia alidai amekuwa haaminiki kwenye Klabu hiyo mbele ya viongozi na baadhi ya wanachama, hivyo hajisikii kuendelea kufanya kazi katika Klabu hiyo.

Katika kipindi cha mwaka mmoja cha kuwa kwake Yanga SC, Kaseja ameidakia mechi 15 tu timu hiyo tangu aliposajiliwa Novemba mwaka jana, akiwa kipa huru baada ya kuachwa na Simba SC, kati ya hizo mechi tano zikiwa za Ligi kuu na Moja ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Kwa ujumla katika mechi hizo, Kaseja amefungwa jumla ya mabao 10, yakiwemo matatu Yanga SC ikilala 3-1 mbele ya mahasimu wao Simba SC, katika mechi ya Nani Mtani jembe Desemba 21 mwaka juzi.