Wednesday , 22nd Jul , 2015

Mabingwa wa ligi kuu Soka Tanzania Bara, Young Africans wanashuka leo kutupa karata yao kwa mara ya pili dhidi ya Telecom ya Djibout katika michuano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.

Mchezo huo utatanguliwa na timu ya Baraza la Halmashauri ya jiji la Kampala KCCA na Adama City Uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam huku Karume ukipigwa mchezo wa Maafande wa KMKM kutoka Zanzibar ikicheza na Khartoum.

Katika mchezo wa hapo jana, Azam FC ya Tanzania imejihakikishia kutinga hatua ya Robo Fainali ya michuano hiyo baada ya kuifunga Malakia ya Sudan bao 2-0 huku Al-Ahly Shandy ya Sudan na LLB AFC ya Burundi zilitoshana nguvu kwa kutoka sare ya bao 2-2 uwanja wa taifa na APR ya Rwanda ikiichapa Heegan ya Somalia bao 2-0 Uwanja wa Karume jijini Dar es salaam.

Kwa matokeo hayo Azam FC iliyopo kundi C inaongoza kundi hilo ikiwa na point sita baada ya mechi ya awali kuilaza KCCA ya Uganda kwa bao 1-0 huku ikifuatiwa na Malakia yenye Pointi tatu.