Thursday , 5th May , 2016

Waamuzi na kamishna watakaochezesha mchezo wa kuwania kucheza hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho kati ya Yanga dhidi ya Sagrada Esperanca ya Angola wanatarajiwa kwuasili hapo kesho.

Afisa Habari wa Shirikisho la Soka nchini TFF Alfred Lucas amesema waamuzi wa mchezo huo wanatoka nchini Ghana ambao watawasili alfajiri ya saa saba usiku huku Kamishna wa mchezo huo ambaye ni Asfaw Luleseged Begashaw kutoka Ethiopia akiwasili kesho mchana.

Lucas amesema, waamuzi wa mchezo huo ni Joseph Odartei Lamptey atakayepuliza filimbi akisaidiwa na washika vibendera David Laryea na Malik Alidu Salifu.

Kwa upande mwingine Lucas amesema, kikosi cha timu ya Esperanca kitawasili leo saa tatu usiku tofauti na hapo awali ambapo walitoa taarifa kuwa watawasili leo saa kumi na moja jioni na hiyo ni kutokana na hali ya hewa ya nchini Angola ambapo kunamvua iliyochangia ndege kuchelewa kuanza safari.

Mchezo huo unatarajiwa kupigwa jumamosi ya Mei 7, Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Mchezo wa marudiano utachezwa Mei 17 mwaka huu Uwanja wa Sagrada Esperanca, zamani ukiitwa Quintalao do Dundo nchini Angola huku marefa kutoka nchini Madagascar wakichezesha mchezo huo.

Waamuzi katika mchezo wa marudiano ni Hamada el Moussa Nampiandraza atakayepuliza filimbi, akisaidiwa na washika vibendera Velomanana Ferdinand Jinoro na Jean Thierry Djaonirina.

Yanga imeangukia katika kapu la, baada ya kutolewa na Al Ahly ya Misri katika hatua ya 16 Bora ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwa jumla ya mabao 3-2, ikilazimishwa sare ya 1-1 Dar es Salaam na kufungwa 2-1 Alexandria.