Tuesday , 3rd Feb , 2015

Nchi nne kati ya sita alikwa zinatarajia kushiriki michuano ya judo kanda ya tano inayotarajiwa kufanyika Februari 10 hadi 15 Mjini Moshi.

Akizungumza na East Africa Radio, Katibu mkuu wa Chama cha Judo nchini JATA, Innocent Malya amesema nchi zilizohakiki kushiriki michuano hiyo ni Kenya, Zanzibar, Burundi, Rwanda na wenyeji Tanzania ambapo amesema nchi mbili za Ethiopia na Rwanda bado hazijahakiki ushiriki wao lakini wanategemea kupata majibu juu ya ushiriki huo mapema kabla ya kuanza kwa michuano hiyo.

Malya amesema, michuano hiyo itashirikisha washiriki 103 kutoka katika nchi hizo ambazo mpaka sasa zimehakiki ushiriki na wataanza kupima uzito Februari 13 kwa wale wanaoanza mashindano Februari 14 huku wale watakaocheza Februari 15 watapima Februari 15.

Malya amesema, kwa upande wa Tanzania, Timu imeshaungana kwa ajili ya kambi iliyopo Mjini Moshi chini ya Kocha Zaid Khamis ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya mashindano hayo ambapo wanatarajia kuchukua ushindi.