Wednesday , 12th Dec , 2018

Msemaji wa klabu ya soka ya Yanga, Dismas Ten, amemtaka mlinzi wa kulia wa timu ya Nkana Red Devils ya Zambia, Hassan Kessy aifunge Simba kwenye mchezo wa klabu bingwa Afrika Jumamosi hii.

Kushoto ni Dismas Ten na kulia ni Hassan Kessy

Dismas kupitia ukurasa wake wa Instagram ametoa ujumbe kwa Hassan Kessy ambaye alijiunga na Nkana mwezi Julai akiwa mchezaji huru baada ya kumaliza mkataba wake na Yanga.

''Kila la kheri Hassan Kessy, wafunge hao bao kama hili'', umesomeka ujumbe wa Dismas ulioambatana na Video ya soka ikionesha goli.

Simba ambayo imeondoka nchini leo kuelekea Kitwe Zambia, itakutana na Nkana jumamosi hii Desemba 15, 2018 kwenye mchezo wa raundi ya kwanza hatua ya kwanza ya klabu bingwa Afrika.

Kitendo cha Dismas kumtaka Kessy aifunge Simba ni mwendelezo wa upinzani wa jadi wa klabu mbili kongwe nchini za Simba na Yanga ambapo katika mchezo wa kwanza wa Simba dhidi ya Mbabane Swallows pia mashabiki wa Yanga waliishangilia timu hiyo kutoka eSwatini.