Wednesday , 7th May , 2014

Upande wa utetezi wa kesi ya mwanariadha Oscar Pistorius ya kumuua aliyekuwa mpenzi wake, Reeva Steenkamp, leo umeendelea kuita mashahidi zaidi, kujaribu kumnasua mwanariadha huyo mlemavu, katika kesi ya mauaji inayomkabili.

Oscar Pistorius

Hii leo mtaalam wa milipuko na risasi, aliitwa kutoa ushahidi, baada ya jana shahidi ambaye ametambulishwa kwa jina Johan Stander, kusema kuwa siku ya tukio alipofika kwa Pistorius, alimkuta akiwa na majuto na uchungu mwingi, alitaka sana kumuokoa marehemu na alichofanya ni kumuomba Mungu tu, kitu kinachoashiria kuwa hakumuua kwa makusudi.

Ushahidi unaotolewa sasa, ni nafasi pekee ya Pistorius na wawakilishi wake kujaribu kumshawishi jaji anayesikiliza kesi hii kuwa, ni kweli alikuwa anajaribu kulinda usalama wake, wakati akifyatua risasi mara nne, kupitia mlango wa chooni kwake uliokuwa umefungwa na kumuua mpenzi wake, akidhani kuwa alikua akimshambulia mhalifu aliyeingia nyumbani kwake.