Tuesday , 23rd Dec , 2014

Jeshi la Polisi Mkoani Tabora limewakamata watu wawili wanaojihusisha na utengenezaji wa silaha za moto aina ya magobole, zinazohusika katika uhalifu.

ACP Suzan Kaganda

Katika msako unaoendeshwa na jeshi la polisi mkoani Tabora ili kuhakikisha wananchi wanasherehekea sikukuu za Krismas na mwaka mpya kwa amani na utulivu, jeshi hilo limefanikiwa kuwatia mbaroni watu wawili wanaojihusisha na utengenezaji wa silaha za moto aina ya magobole Tisa zinazohusika katika uhalifu.

Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari mkoani Tabora kamanda wa Polisi kamishna msaidizi ACP Suzani Kaganda amesema kuwa, imekamatwa pia mitambo ya kutengenezea pombe haramu ya moshi, ambapo watuhumiwa wa silaha wamekiri kujihusisha na utengenezaji na uuzaji wa silaha hizo ambazo zimekuwa zikitumika katika uhalifu.

Aidha baadhi ya wananchi walioongea na EATV pamoja na kero ya unyang’anyi wa kutumia silaha, wamesema kuwa, pale wanapobainika watuhumiwa kama hao wanaojihusisha na matukio ya uhalifu adhabu zinazotolewa na vyombo husika zinaonekana kutokidhi matakwa ya matukio na ndio maana matukio yanaongezeka siku hadi siku.