Tuesday , 28th Oct , 2014

Watu watano wakazi wa mkoa wa Singida wamefariki dunia katika matukio matatu tofauti likiwemo la watu wawili kuzama katika bwawa la maji wilayani manyoni.

Akieleza matukio hayo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida Kamishina Msaidizi wa jeshi la Polisi bwana Thobias Sedoyeka, amesema tukio la kwanza watu wawili wamezama katika bwawa lililoko katika kijiji cha Agondi wilayani Manyoni wakati wakiogelea, tukio lingine mwanafunzi aliye maliza darasa la Saba, ambaye alikuwa amepanda baiskeli amegongwa na gari la mizigo katika kijiji cha kibigiri wilayani Iramba kwenye barabara kuu itokayo Singida kuelekea mwanza.

ACP Sedoyeka amesema  tukio la mwisho ni watu wawili wamefariki  katika kijiji cha mwamatiga wilayani Manyoni baada ya Bwana Bhija Jandika  kumchoma kisu Bwana Shija Masele katika kilabu cha pombe na hatimaye watu wenye hasira  kuamua kujichukulia sheria mkononi na kumpiga Bwana Shija Masele kwa mawe na magongo na kusababisha kifo chake.

Kwa upande wao waokoaji na mashuhuda waliofika kutoa msaada  wamesema pamoja na kwamba bwawa hilo limekuwa msaada mkubwa katika kijiji chao kwa kuchota maji kwa ajili ya matumizi ya kawaida pamoja na mifugo kunywa ,imefika wakati sasa wazazi kuwaelimisha vijana wao kuacha kuogelea katika bwawa hilo ,ni hatari kwasababu lina kina kirefu pia lina mawe  yenye incha kali.

Bwawa la Aghondi ambalo lina hudumia wananchi zaidi ya watu  Elfu Mbili wa vijiji viwili vya   Aghondi na kaminyanga wilayani Manyoni, lina chemchem ambayo inatoa maji chini ya ardhi   na mazuri kwa ajili ya matumizi ya binadamu na mifugo , bwawa hilo limetokea baada ya mkandaras wa kampuni ya CGC iliyokuwa ikijenga barabara kuu ya lami kutoka Manyoni hadi Singida kuchimba kokoto sehemu hiyo.