Rais wa Mahakama ya Afrika na Haki za Binadamu iliyopo mjini Arusha Jaji Augustino Ramadhani
Maeneo muhimu yatakayotiliwa mkazo katika kongamano hilo la wiki moja ni pamoja na usimamizi wa kesi zinazojirudia na mchakato wa kumaliza mashauri kwa njia ya maelewano.
Wataalamu hao ambao ni pamoja na Mkuu wa idara ya sheria wa ECHR bwana Attila Teplan na mkuu wa huduma za teknelojia ya habari na mawasiliano Bw. John Hunter, watabadilishana uzoefu na wenzao wa mahakama ya Afrika ya haki za binadamu na watu kuhusu namna bora ya uendeshaji wa mashauri yanayohusu haki za binadamu .
Hatua hiyo ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 10 ya mahakama ya Afrika ya haki za binadamu na watu ambapo mwaka 2016 umetangazwa kuwa ni mwaka wa umoja wa Afrika wa haki za binadamu huku mkazo mahsusi ukiwa katika haki za wanawake na watoto.
Akizungumza katika kongamano hilo, Msajili wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na watu Dk. Robert Eno alisema hatua ya kubadilishana uzoefu itainua na kuimarisha urafiki na mshikamano uliopo baina ya Mahakama hizo
“Jambo hili litafungua milango ya kuona maeneo mapya ya ushirikiano katika nyanja ya sheria baina ya taasisi hizi zetu mbili," alisema Dk. Eno.
Dk. Eno aliahidi utayari wa AfCHPR kujifunza kutoka mahakama ya Ulaya ya Haki za Binadamu ili kupata uzoefu wa kuboresha utekelezaji wa shughuli za Mahakama .
Mahakama ya Ulaya ya haki za binadamu yenye makao yake makuu katika mji wa Strasbourg nchini Ufaransa ilianzishwa mwaka 1959 na ina uzoefu wa zaidi ya miaka 50 imekishwa toa hukumu zaidi ya 10,000 zinazohusu ukiukwaji wa mkataba wa Ulaya kuhusu haki za Binadamu.
Kwa upande wake Mahakama ya Afrika ya haki za binadamu na watu ilianzishwa kwa mujibu wa kifungu namba moja cha itifaki ya mkataba wa mahakama hiyo ili kuimarisha jukumu la kulinda haki za tume ya Afrika ya Haki za Binadamu na watu barani Afrika ambapo itifaki hiyo ilikubaliwa Juni 1998 nchini Burkina Faso na ikaanza kutumika Januari 25, 2004 na kuridhiwa na zaidi ya nchi 15 wanachama wa Umoja wa Afrika.