Thursday , 23rd Oct , 2014

Vijana wanaoendesha kampeni ya IPTL Bring Back Our Money, au Kiswahili IPTL Rudisha Pesa za Umma, wametishia kuandamana hadi ofisi za Shirika la Fedha Ulimwenguni IMF jijini Dar es Salaam, kushinikiza shirika hilo lisitoe mkopo kwa Tanzania.

Kiongozi wa kundi la Vijana wanaoendesha kampeni ya IPTL Bring Back Our Money, Bw. Ben Sanane.

Mkopo huo ni ule ambao vijana hao wanadai kuwa serikali ya Tanzania imekopa kwa IMF, katika harakati zake za kutaka kufidia nakisi inayotokana na wahisani kusitisha msaada wao wa kibajeti kwa Tanzania unaofikia shilingi bilioni 972 kufuatia sakata la IPTL na tuhuma za ufisadi katika akaunti ya Escrow ya Benki Kuu ya Tanzania .

Wakizungumza jijini Dar es Salaam leo, vijana hao wakiongozwa na Ben Sanane wamesema haitakuwa vema kwa IMF kukubali kutoa mkopo huo, kwani kitendo hicho watakitafsiri kuwa ni kubariki vitendo vya ufisadi na kuwakumbatia wafujaji wa pesa za walipa kodi Watanzania maskini.

Kwa mujibu wa vijana hao, IMF ilitakiwa kuungana na Watanzania kwa kukataa kutoa fedha hizo wanazodai kuwa zitatakiwa kulipwa na watanzania wale wale ambao sasa wanalalamika kuwa fedha zao zimechukuliwa kupitia sakata la IPTL.