Thursday , 14th May , 2015

Waganga wa tiba asili elfu sabini na moja, wanaojishughulisha na utoaji wa tiba asili na tiba mbadala, wanafanya kazi zao pasipo kutambulika na mamlaka zozote nchini Tanzania kiasi cha kufanya zoezi la kukabiliana na imani potofu ikiwemo ramli.

Hali hiyo imebainika jijini Dar es Salaam katika mkutano baina ya waandishi wa habari na Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala, wakati baraza hilo lilipotangaza kuondoa zuio la matangazo ya tiba asili na tiba mbadala ililolitoa mwaka jana kufuatia madai ya kukiukwa kwa taratibu za utoaji wa matangazo hayo.

Akijibu swali kutoka kwa mwandishi wa East Africa Radio, Mratibu wa Tiba Asili na Tiba Mbadala wa Wilaya na Mikoa amesema kuwa kati ya watoa tiba asili na tiba mbadala sabini na saba elfu, ni watoa tiba elfu sita tu ndiyo wamesajiliwa na baraza hilo lililo chini ya Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii.

Kuhusu matangazo ya tiba asili na tiba mbadala, Bi. Bakari amevitaka vyombo vya habari kuzingatia taratibu na miiko inayosimamia utangazaji, huku watoa tiba asili na wao wakipewa sharti la kuhakikisha kuwa matangazo yao yanapelekwa kwenye baraza hilo kwa kukaguliwa kabla ya kurushwa au kutangazwa katika vyombo vya habari husika.