Saturday , 19th Mar , 2016

Uharibifu wa njia za wanayamapori maarufu kama SHIROBA ambazo ni mapitio ya wanyama na maeneo ya kuzaliana umekua tishio kwa uhifadhi endelevu kutokana na njia hizo kuingiliwa na shughuli za binadamu ikiwemo kilimo,ujenzi wa makazi ya watu.

Kaimu Mhifadhi Mkuu wa Hifadhi ya Manyara Ibrahim Ninga

Hayo yameelezwa na Kaimu Mhifadhi Mkuu wa Hifadhi ya Manyara Ibrahim Ninga ambaye amesema kuwa maeneo mengi ya mapitio ya wanyama yako nje ya hifadhi na yanamilikiwa na serikali za mitaa ambapo yamekua yakiuzwa kiholela kwa watu binafsi na wawaekezaji ambao hujenga hoteli na kukwamisha ikolijia ya wanyama .

Mhifadhi huyo akizungumza na waandishi wa habari katika ziara ya waandishi wa habari waliotembelea ziwa Manyara ,ziara iliyoandaliwa na Tanapa,Ibrahim amesema kuwa licha ya kuanzishwa kwa sheria ya kulinda njia za wanayamapori bado hakuna kanuni zinazosimamia sheria hiyo jambo ambalo linatoa mwanya kwa njia hizo kuharibiwa na binadamu.

Ibrahim amesema kuwa hatua ya serikali kuweka tozo za pamoja kwa wananchi wa jumuiya ya Afrika Mashariki itasaidia kuinua utalii wa ndani na kuongeza idadi kubwa ya watalii hivyo amewataka wananchi kuchangamkia fursa ya kutembelea hifadhi ya Manyara.

Kwa upande wao Wanahabari kutoka vyombo mbalimbali vya habari waliotembelea Hifadhi hiyo ,Pamela Mollel na Onesmo Loi wamesema kuwa umoja wa forodha na tozo zinazofanana kwa nchi za jumuiya ya Afrika Mashariki katika vivutio vya utalii itatoa fursa kwa wanajumuiya wote kuzifikia hifadhi kwa gharama nafuu.

Hifadhi ya Ziwa Manyara inasifika kwa kuwa na idadi kubwa ya viboko,chemichemi za maji moto pamoja na wanayama pori wakiwemo samba wapandao miti,pundamilia na twiga pamoja na Tembo.