Friday , 19th Dec , 2014

Asasi isiyo ya kiserikali iliyoasisiwa na Mke wa Balozi wa Uturuki nchini inakusudia kujenga kijiji maalum cha kuwahifadhi na kuwaendeleza kitaaluma, kibiashara na kiufundi watu wenye ulemavu wa ngozi-(Albinism).

Hayo yamebainika jijini Dar es Salaam wakati Balozi wa Uturuki nchini Mhe. Ali Davutoglu na mkewe Bi Yesim Mego Davutoglu walipomtembelea ofisini kwake Mwenyekiti Mtendaji wa IPP Dr Reginald Mengi.

Wakati wa Mazungumzo hayo Bi Yesim Davutoglo amesema anasikitishwa na unyanyapaa na mauaji wanayofanyiwa watu wenye ulemavu wa ngozi nchini, na ili kusaidia kulinda uhai wao asasi yake pamoja na wadau wake kwa kushirikiana na serikali ya Tanzania itaanza ujenzi wa kijiji cha kuwatunza na kuwaendeleza kielimu mapema mwakani, na tayari eneo la meta za mraba 35,000 limeshapatikana jirani na mji wa Bagamoyo.

Akizungumzia mahusiano ya kibiashara baina ya Uturuki na Tanzania, Balozi wa Uturuki Mhe. Ali Davutoglo amesema ni mzuri na unazidi kuimarika kila mwaka.

Kwa upande wake Mwenyekiti Mtendaji wa IPP Dr Reginald Mengi, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania –TPSF ameipongeza Uturuki kwa kufanyabiashara na Watanzania kwa malengo ya kuunufaisha kila upande, na kusisitiza kuwa ni fikra potofu kudhani kuwa fedha ndiyo mtaji pekee unaohitajika katika uwekezaji.